Mo Salah ang'ara huku Liverpool ikiicharaza Roma 5-2
Mchezo wa kiwango cha kipekee wa Mohamed Salah uliisaidia Liverpool kuchukua udhibiti wa nusu fainali ya kombe la vilabu bingwa Ulaya-lakini mabao 2 ya dakika za lala salama ya Roma yaliipatia timu hiyo ahueni katika duru ya pili ya kombe hilo.
Liverpool ambao pia walifanikiwa kufika fainali ya 2007, waliipita safu ya ulinzi ya Roma bila pingamizi na kufunga mara tano katika dakika 68 za kipindi cha kwanza na cha pili katika uwanja wa Anfield.
Salah ambaye kwa sasa amefunga mabao 43 tangu ahamie Liverpool kutoka Roma alifunga mabao mawili na kutoa usaidizi wa mabao mawili.
Aliuficha mpira katika kona ya goli kabla ya kumfunga tena kwa ustadi kipa Alisson kwa bao lake la pili.
Salah baadaye alipata mpira akatamba kabla ya kumpatia Sadio Mane pasi murua na kufanya mambo kuwa 3-0, kabla ya kutoa pasi nyengine kama hiyo kwa mshambuliaji Robert Firminio aliyefunga bao la nne.
Liverpool baadaye ilikuwa timu ya pili kufunga mabao matano katika mechi ya nusu fainali ya kombe la vilabu bingwa Ulaya wakati Firmino alipofunga kwa kichwa kona iliopigwa na James Milner.
Huku timu yake ikiongoza 5-0 baada ya dakika 68, Mkufunzi wa Liverpool Jurgen Klopp alimuondoa Salah na Roma ikajipatia fursa katika mechi ya marudio wiki ijayo katika uwanja wa Stadio Olimpico.
Kwanza Eden Dzeko aliifungia timu yake bao la kwanza kutoka kwa pasi ya Radja Nainggolan na baadaye Diego Perotti alifunga mkwaju wa penalti baada ya Milner kuunawa mpira katika eneo hatari.
Sasa Roma itahitajika kutumia kila mbinu ili kushinda 3-0 nyumbani Italy ili kusonga katika fainali ya kombe hilo.
Wiki mbili zilizopita Roma iliwashangaza mabingwa wa Uhispania Barcelona kwa kuwalaza 3-0 baada ya Barcelona kuicharaza timu hiyo 4-1 katika duru ya kwanza.
Iwapo watafanikiwa kuilaza Liverpool nyumbani basi wataingia katika fainali dhidi ya Bayern Munich ama Real Madrid ambao wanakutana Jumatano kwa mechi nyengine ya nusu fainali.
Mbali na mabao mawili yaliofungwa na Roma katika kipindi cha pili cha mechi kiungo wa kati wa Liverpool Alex Oxlaide-Chamberlain alitolewa uwanjani kwa machela baada ya kupata jereha.
Kocha Jurgen Klopp anasema kuwa huenda kiungo huyo alipata jeraha 'baya sana'.