Got a TV Licence?

You need one to watch live TV on any channel or device, and BBC programmes on iPlayer. It’s the law.

Find out more
I don’t have a TV Licence.

Habari za moja kwa moja

Na Asha Juma

time_stated_uk

  1. Israel-Gaza: Mtoto aokolewa kutoka kwa tumbo la mama aliyekufa baada ya shambulio la Israeli

    .

    Sabreen alikuwa amekufa kabla kumtazama machoni mwanawe au kumbeba.

    Mama huyo mwenye umri mdogo alikuwa amebeba mtoto wake kwa miezi saba na nusu ya ujauzito.

    Zilikuwa siku zenye hofu ya kila mara, lakini Sabreen alitumaini kwamba bahati ya familia hiyo ingedumu hadi vita viishe.

    Bahati hiyo ilitoweka kutokana na kishindo na moto wa mlipuko saa moja kabla ya saa sita usiku tarehe 20 Aprili.

    Waisraeli walirusha bomu kwenye nyumba ya familia ya al-Sakani huko Rafah ambapo Sabreen, pamoja na mumewe na binti mwingine wa wanandoa hao - Malak wa miaka mitatu - walikuwa wamelala.

    Sabreen alipata majeraha makubwa na mumewe na Malak waliuawa, lakini mtoto alikuwa bado hai tumboni mwa mamake wakati waokoaji walipofika eneo hilo.

    Walimkimbiza Sabreen hospitalini, ambapo madaktari walimfanyia upasuaji wa dharura ili kujifungua mtoto.

    Sabreen hakuweza kuokolewa lakini madaktari walifanya kazi ya kumfufua mtoto, wakigonga kifua chake taratibu ili kuamsha kupumua.

    Hewa ilisukumwa kwenye mapafu yake."Alizaliwa katika hali mbaya ya kupumua," Dkt Mohammed Salama, mkuu wa kitengo cha dharura cha watoto wachanga katika Hospitali ya Emirati huko Rafah.

    Lakini mtoto huyo - ambaye alikuwa na uzani wa kilo 1.4 tu (pauni 3.1) - alinusurika na mateso ya kuzaliwa kwake.Daktari aliandika "mtoto wa shahidi Sabreen al-Sakani" kwenye kipande cha kanda na kukiambatanisha na mwili wake.

    Kisha akawekwa kwenye incubator."Tunaweza kusema kuna maendeleo fulani katika hali yake ya afya," Dk Salama alisema.

  2. Uchaguzi wa Afrika Kusini: ANC yashindwa kupigania jina na nembo ya chama cha MK cha Jacob Zuma

    .
    Image caption: Nembo ya mkuki ni sawa na ile inayotumiwa na mrengo wa sasa wa ANC

    Chama cha African National Congress (ANC) cha Afrika Kusini kimepoteza jitihada za kisheria kukizuia chama kipya kutumia jina na nembo ya mrengo wake wa zamani.

    Chama tawala cha ANC kilidai kuwa uMkhonto we Sizwe (MK), kinachoongozwa na Rais wa zamani Jacob Zuma, kilikuwa kimekiuka sheria ya nembo ya biashara.

    Lakini Mahakama Kuu ya Durban iliruhusu matumizi ya jina hilo, linalotafsiriwa kama Spear of the Nation.Ni ushindi muhimu kwa MK kabla ya uchaguzi mkuu wa Mei 29.Wafuasi wa Bw Zuma walishangilia na kuimba mahakamani baada ya hukumu kutolewa.

    Chama cha ANC kimesema kitakata rufaa dhidi ya uamuzi huo.

    Mwezi uliopita, ANC ilipata pigo lingine la kisheria katika jaribio lake la kukizuia MK kushiriki uchaguzi, kikisema kuwa hakijatimiza vigezo rasmi vya kujiandikisha.

    Jina na nembo ya MK ina ishara kubwa ya kisiasa kwa sababu ya jukumu la mrengo huo ambao haupo tena katika kupigania kukomesha utawala wa wazungu wachache nchini Afrika Kusini.

    Chama kipya cha MK kinaweza kukosa nafasi ya kushinda uchaguzi, lakini kuna uwezekano wa kuathiri pakubwa ANC, ambacho, kwa mara ya kwanza tangu kumalizika kwa utawala wa kibaguzi mwaka 1994, kinaweza kupoteza wingi wake wa wabunge bungeni.

  3. Mechi yasitishwa kufuatia mgogoro wa ramani ya Morocco katika jezi

    .

    Mechi ya kwanza ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la Caf kati ya USM Alger na Renaissance Berkane ya Morocco haikufanyika Jumapili kwa sababu ya mzozo wa jezi.

    Ukanda wa jezi wa timu ya Berkane una ramani ya Morocco iliyopanuliwa, ambayo inajumuisha eneo linalozozaniwa la Sahara Magharibi.

    Algeria inaona ramani hiyo, ambayo imeonyeshwa katikati ya shati, kama uchochezi na maafisa wa forodha waliichukua jezi hiyo wakati klabu hiyo ya Morocco ilipowasili nchini humo siku ya Ijumaa.

    Berkane wamekuwa wakitumia jezi hiyo hiyo katika msimu huu wote wa mashindano - pamoja na muundo kama huo katika kampeni za awali za bara - na Shirikisho la Soka la Afrika (Caf) liliidhinisha haki yao ya kuivaa jezi hiyo baada ya mkutano ulioitishwa kwa haraka baina ya kamati ya klabu.

    Pande zote mbili zilisafiri hadi uwanjani tayari kwa mechi hiyo , USM Alger wakaelekea uwanjani , lakini wageni walibaki kwenye chumba chao cha kubadilishia nguo.

    Taarifa ya Caf, ilisema suala hilo "litapelekwa kwa vyombo husika".

    Baraza tawala pia lilitoa pole kwa wafadhili, washirika wa TV na wafuasi kwa usumbufu wowote uliojitokeza.

    USM Alger ndio watetezi wa Kombe la Shirikisho, ambalo lilikuwa la daraja la pili la mashindano ya bara kabla ya kuanzishwa kwa Ligi ya Soka ya Afrika, wakati Berkane ilinyakua taji hilo mnamo 2020 na 2022.

    Mechi ya mkondo wa pili wa nusu fainali imepangwa kufanyika mjini Berkane Jumapili, Aprili 28.

    Mvutano kati ya Algeria na Morocco umekuwa mgumu kwa miaka mingi, huku Algeria ikikata uhusiano wa kidiplomasia mnamo 2021.

  4. Watu 13 wafariki kwa ajali ya gari nchini Tanzania

    Ajali

    Watu 13 wamefariki dunia na wengine 6 wamejeruhiwa kutokana na ajali ya gari.

    Basi dogo la abiria aina ya Coaster iliyokuwa inatoka eneo la Somanga kuelekea Kilwa Kivinje, mkoni Lindi liligongana uso kwa uso na Lori la mafuta.

    Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Lindi, John Imori amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo.

    Taratibu za kubaini chanzo cha ajali hiyo zinaendelea.

  5. Wimbo 'Zakayo' wa mwimbaji wa Tanzania wazua mjadala Kenya

    .
    Image caption: Baadhi ya Wakenya walikisia kwamba wimbo huo huenda unamhusu rais wao

    Mmoja wa wanamuziki maarufu wa nyimbo za Injili Afrika Mashariki, Christina Shusho, amezua mjadala nchini Kenya baada ya kuachia kionjo cha wimbo wake mpya kwa jina Zakayo.

    Baadhi ya Wakenya, ambako mwimbaji huyo wa Tanzania ana wafuasi wengi, wamehisi kwamba wimbo huo unamhusu Rais wa Kenya, William Ruto.

    Baadhi ya Wakenya kwa dhihaka humtaja Rais Ruto kama Zakayo - Kiswahili kwa mtu anayetajwa katika Biblia, ambaye anajulikana kuwa mtoza ushuru aliyepanda juu ya mti ili kumwona Yesu.

    Kwa Kiswahili, Shusho anaimba, "Kulikuwa na mtu mmoja jina lake Zakayo, mkuu wa watoza ushuru na tajiri, alitafuta kuona Yesu ni mtu wa aina gani...

    "Bw Ruto alipata jina la utani Zakayo kwa sababu ameanzisha mikakati mingi ya kutoza ushuru mpya, tangu achaguliwe rais mnamo Agosti 2022.

    Hilo limemfanya kutopendwa na Wakenya wengi wanaoamini kuwa amesaliti ahadi yake ya kampeni ya kutetea masilahi ya "hustlers" – Wakenya walio wanyonge kifedha .

  6. Urusi yapinga msaada mpya wa Marekani kwa Ukraine

    .

    Sheria iliopo tangu Urusi ilipovamia Ukraine kwa kiwango kikubwa ni kwamba kile ambacho ni kizuri kwa Kyiv ni kibaya kwa Moscow.

    Jumamosi iliyopita ilileta habari njema kwa serikali ya Ukraine.

    Bunge la Wawakilishi la Marekani lilipiga kura kuunga mkono kifurushi cha msaada cha $61bn (£49bn) kwa Kyiv, ambacho kitatumika kulipatia jeshi lake silaha.

    Bunge pia liliidhinisha muswada ambao utaruhusu kukamatwa na kuhamishiwa Ukraine mali ya Urusi iliyohifadhiwa Marekani.

    Miswada hiyo sasa inapelekwa kwa Seneti ili kuidhinishwa.

    Haishangazi, ni kwanini hatua hii haikupokelewa vyema mjini Moscow.Rais wa zamani Dmitry Medvedev alilaani "dola bilioni 61 za umwagaji damu".

    Alitoa wito wa kuwepo kwa Vita vipya vya Wenyewe kwa Wenyewe kwa Waamerika ambavyo "hatimaye vitasababisha kuvunjika vibaya kwa himaya ya uovu ya Karne ya 21, Marekani".

    Katika kipindi chake kikuu cha televisheni cha serikali Jumapili usiku, mtangazaji Vladimir Solovyov alielezea wazo la kuhamisha mali ya Urusi hadi Ukraine kama "kitendo cha ugaidi wa kifedha".

    "Ikiwa watapitia hili," Bw Solovyov alisema, "basi katika ngazi ya Jimbo la Duma na serikali, lazima tuitangaze Marekani kuwa gaidi wa kifedha."

    Aliongeza kuwa sasa anaamini vita kati ya Urusi na Nato "haviwezi kuepukika".

  7. Daktari anayehusishwa na kundi la Islamic State ahukumiwa miaka 12 jela

    Daktari wa Kenya anayehusishwa na kundi la kigaidi la Islamic State amehukumiwa miaka 12 jela kwa kupanga shambulio kubwa la kibaiolojia yapata miaka minane iliopita.

    Mohammed Abdi Ali alikuwa anapanga kutumia virusi vya kimeta kutekeleza shambulio hilo lakini alikamatwa kufuatia taarifa ya wananchi kwa polisi.

    Ali pia alikuwa na hatia ya kuwahusisha vijana hao na wapiganaji wengine wa Islamic State nchini Libya.

    Alikamatwa pamoja na watu wengine wawili ambao waliachiliwa kwa kukosa ushahidi.

    Hakimu alisema kwamba alizingatia miaka 8 aliyokuwa gerezani.

  8. Mkuu wa kurugenzi ya ujasusi katika jeshi la Israel ajiuzulu kutokana na shambulio la Oktoba 7

    ,

    Mkuu wa kijasusi wa jeshi la Israel amejiuzulu, akisema alichukua jukumu la kushindwa kabla ya shambulio la Hamas dhidi ya Israel tarehe 7 Oktoba.

    Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) lilisema Meja Jenerali Aharon Haliva atastaafu pindi mrithi wake atakapochaguliwa.

    Katika barua, alikiri kwamba kurugenzi yake ya ujasusi "haikutimiza kazi tuliyokabidhiwa".

    Yeye ndiye mtu wa kwanza mkuu kujiuzulu kutokana na shambulio hilo ambalo lilikuwa baya zaidi katika historia ya Israel.

    Wanajeshi na maafisa wa ujasusi wa Israel walikosa au kupuuza maonyo mengi kabla ya mamia ya watu wenye silaha wa Hamas kuvunja uzio wa mpaka wa Gaza siku hiyo na kushambulia jamii za karibu za Israel, kambi za kijeshi na tamasha la muziki.

    Takriban Waisrael 1,200 na raia wa kigeni - waliuawa na wengine 253 walirejeshwa Gaza kama mateka, kulingana na hesabu za Israel.

    Israel ilijibu kwa kuanzisha vita vyake vikali zaidi kuwahi kutokea Gaza kwa malengo ya kuangamiza Hamas na kuwakomboa mateka.

    Zaidi ya Wapalestina 34,000 huko Gaza - wengi wao wakiwa watoto na wanawake - wameuawa katika mzozo huo, wizara ya afya ya eneo hilo inayoendeshwa na Hamas inasema.

    Pia unaweza kusoma:

    Netanyahu aapa kukataa vikwazo vyovyote kwa jeshi la Israel

  9. Takriban mapipa bilioni 10 ya mafuta yagunduliwa pwani ya Namibia

    .

    Takriban mapipa bilioni 10 ya mafuta yamegunduliwa nchini Namibia, kampuni ya mafuta ya Ureno ya Galp Energia imesema.

    Kampuni hiyo ilifichua uwezo huo baada ya kuhitimisha awamu yake ya kwanza ya utafutaji wa mafuta katika uwanja wa Mopane pwani ya Namibia.

    "Katika eneo la Mopane pekee, na kabla ya kuchimba visima vya ziada vya uchunguzi na tathmini, makadirio ya mahali pa hidrokaboni ni sawa na mapipa bilioni 10 ya mafuta, au zaidi," ilisema Jumapili.

    Akiba kubwa ya mafuta na gesi imegunduliwa katika Bonde la Machungwa nchini Namibia, ambako Mopane iko, katika miaka ya hivi karibuni.

    Ugunduzi huo umeiweka nchi hiyo ya kusini mwa Afrika kama mhusika mkuu katika sekta ya mafuta duniani.

    Nchi inatazamia kuingia kwa shirika la wazalishaji wa mafuta la Opec kabla ya kuanza kwa uzalishaji wa mafuta mnamo 2030.

  10. Saba wafariki wakati gari la mbio za magari lilipogonga umati wa watu

    .

    Watu saba wamefariki na wengine 21 kujeruhiwa baada ya gari la mashindano ya mbio kuwagonga watazamaji katika hafla ya uendesdhaji magari nchini Sri Lanka.

    Ajali hiyo ilitokea katika mbio za Fox Hill Supercross siku ya Jumapili huko Diyatalawa, mji wenye kambi ya jeshi.

    Miongoni mwa waliofariki ni maafisa wanne wa mbio pamoja na watazamaji, akiwemo msichana wa miaka minane, jeshi lilisema.

    Maelezo machache yametolewa kuhusu dereva, hali yake na iwapo atakabiliwa na mashtaka.

    Lakini mamlaka ilisema uchunguzi kamili wa polisi ulikuwa unaendelea kuhusu ajali hiyo iliyotokea kwenye njia inayomilikiwa na jeshi. Diyatalawa, katikati mwa kusini mwa Sri Lanka ni mji wa zamani unaochukuliwa kuwa ngome na jeshi lina chuo chake huko.

    "Ajali hii ilitokea wakati gari liliporuka nje ya njia," msemaji wa polisi Nihal Talduwa alisema, kwa mujibu wa BBC Sinhala.

    Kulingana na mashuhuda, ajali hiyo ilitokea mara baada ya gari lingine kupinduka kwenye njia.

    Maafisa walijaribu kupunguza mwendo wa magari kuzunguka eneo la tukio kwa kuwasha taa za manjano, lakini magari yalipopita kwa kasi, gari moja jekundu lilitoka nje na kuwagonga watazamaji kando ya njia isiyokuwa na walinzi.

  11. Waandamanaji wa Niger watoa wito wa kuondoka mara moja kwa wanajeshi wa Marekani

    ,

    Mamia ya watu wamefanya maandamano huko Agadez kaskazini mwa Niger, wakitoa wito wa kuondoka mara moja kwa wanajeshi 1,000 wa Marekani walioko huko.

    Maandamano hayo ya Jumapili yaliitishwa na mashirika yanayounga mkono mamlaka ya kijeshi ambayo yalichukua uongozi mwaka jana.

    Tukio hilo limefanyika siku mbili baada ya Marekani kukubali kuondoa vikosi vyake katika taifa la Sahel kujibu uamuzi wa mwezi uliopita wa serikali inayoongozwa na jeshi mjini Niamey ya kubatilisha makubaliano yaliyoruhusu majeshi ya Marekani kufanya kazi nchini humo.

    Marekani pia ilikubali kufunga kambi ya ndege zisizo na rubani kutoka eneo ambapo inendesha operesheni dhidi ya makundi ya wapiganaji wa Kiislamu.

    "Ujumbe wetu uko wazi: Wanajeshi wa Marekani, bebeni virago vyenu na muende nyumbani," mmoja wa waandamanaji aliambia shirika la habari la AFP.

    Waandamanaji walionekana wakiwa wamebeba bendera za Urusi, pamoja na Burkina Faso, Mali na Niger.

    Viongozi wa kijeshi katika nchi hizi wamekuwa wakiimarisha uhusiano na Moscow.

    Niger iko katika eneo la Sahel barani Afrika, ambalo linachukuliwa kuwa kitovu kipya cha kimataifa cha kundi la Islamic State.

    Marekani imeitegemea Niger kama kambi yake muhimu kwa kufuatilia shughuli za kikanda za wanajihadi.

    Makumi ya wakufunzi wa kijeshi wa Urusi wamewasili Niger katika wiki za hivi karibuni, wakileta mfumo wa hali ya juu wa ulinzi wa anga, kulingana na ripoti za vyombo vya habari vya serikali.

    Soma zaidi:

    Kwa nini Marekani haiyaiti mapinduzi ya Niger kuwa ni mapinduzi?

  12. Jeshi la Nigeria laapa kulipiza kisasi baada ya wanajeshi kuuawa kwa shambulizi la kuvizia

    .
    Image caption: Jeshi linasema liliua idadi isiyojulikana ya washambuliaji

    Jeshi la Nigeria limeapa kulipiza kisasi kwa mauaji ya wanajeshi sita waliovamiwa wakiwa kwenye misheni ya amani katika jimbo la kati la Niger wiki iliyopita.

    Wanajeshi hao walikuwa kwenye "doria" katika kijiji cha Karaga eneo la Shiroro Ijumaa iliyopita walipovamiwa na wale ambao jeshi liliwaita "magaidi".

    Taarifa ya jeshi ilisema idadi ya washambuliaji wameuawa, na wengine bado wanafuatiliwa.

    Iliapa kwamba "tukio hilo la kusikitisha litalipizwa kisasi na wanajeshi".

    Wanajeshi waliouawa ni pamoja na maafisa wakuu wawili na wafanyikazi wengine wanne, kulingana na jeshi.

    Maafisa wawili walijeruhiwa wakati wa shambulio hilo.

    Jeshi halijathibitisha taarifa za ndani kwamba afisa mmoja alitekwa nyara.

    Haijabainika ni nani alitekeleza shambulio hilo lakini magenge yenye silaha, yanayojulikana na wenyeki kama majambazi, yamelaumiwa kwa kulenga vikosi vya usalama katika mashambulizi ya hivi majuzi.

    Haya yanajiri wakati Nigeria ikiwa mwenyeji wa mkutano wa kilele wa siku mbili wa ngazi ya juu wa Afrika dhidi ya ugaidi katika mji mkuu wa Abuja.

    Shambulizi hilo la kuvizia pia linafanyika wiki chache baada ya wanajeshi wengine 16 kuuawa walipokuwa wakijibu mapigano kati ya jamii zinazohasimiana katika jimbo lenye utajiri wa mafuta kusini mwa Delta.

    Nigeria imekumbwa na wimbi la utekaji nyara kwa lengo la kulipwa fidia, pamoja na kupambana na makundi mbalimbali ya wanajihadi.

    Soma zaidi:

    Wanajeshi sita wa Nigeria wauawa katika shambulizi la kuvizia

  13. Mashambulizi ya Israel bado yanaendelea huko Gaza

    .

    Mashambulizi ya Israel yanaendelea kote Gaza, huku watu saba wakiuawa katika kambi ya wakimbizi ya Nuseirat baada ya siku moja ya milipuko ya mabomu iliyosababisha vifo vya watu 22 kusini mwa mji wa Rafah.

    Mtoto wa kike aliyezaliwa na mwanamke aliyeuawa katika mashambulizi ya Rafah yuko katika hali nzuri, madaktari wanasema.

    Wafanyikazi wamepata miili 180 hadi sasa kutoka kwa kaburi la pamoja lililopatikana baada ya vikosi vya Israel kuondoka katika Hospitali ya Nasser huko Khan Younis, shirika la habari la Al-Jazeera limesema.

    Kiongozi Mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei alisema "cha muhimu zaidi ni kwamba Iran ilionyesha uwezo wake" katika shambulio la ndege zisizo na rubani na makombora la Iran dhidi ya Israel.

    Soma zaidi:

    Netanyahu aapa kukataa vikwazo vyovyote kwa jeshi la Israel

  14. Israel yachunguza kifo cha mhudumu wa afya katika Ukingo wa Magharibi

    .

    Jeshi la Israel limeanzisha uchunguzi baada ya mhudumu wa kujitolea wa Kipalestina kuuawa katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu.

    Shirika la Red Crescent la Palestina lilisema Mohammed Awad Allan, 50, alipigwa risasi alipokuwa akiwatibu watu waliokuwa wamejeruhiwa na walowezi wa Israel.

    Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) limesema vikosi vilitumwa katika kijiji cha As-Sawiya ili kuzima mapigano.

    Ilithibitisha kuwa dereva wa gari la wagonjwa aliuawa, na tukio hilo linachunguza.

    Mazingira ya kifo hayako wazi.

    Katika taarifa ya Jumapili, IDF ilisema wanajeshi na vikosi vya Polisi vya Mipakani vya Israel vilitumwa kufuatia ripoti za "makabiliano makali ya kurushiana mawe yaliyotokea kati ya Wapalestina na raia wa Israel katika eneo la As-Sawiya".

    Iliongeza: "Wakati wa tukio hilo, dereva wa gari la wagonjwa la Palestina la Red Crescent aliuawa. Polisi wa Kijeshi wameanzisha uchunguzi."

    Bw Allan alijaribu kuwatibu watu waliojeruhiwa "na milio ya risasi iliyofyatuliwa na walowezi wa Israel".

    Baadhi ya ripoti za vyombo vya habari vya lugha ya Kiebrania zilisema Bw Allan aliuawa kwa kupigwa risasi na wanajeshi wa Israel - zingine ziliripoti alipigwa risasi na walowezi waliokuwa na silaha.

    Soma zaidi:

    Shambulizi la Israel Iran: Uharibifu waonekana katika kambi ya anga ya Isfahan

  15. Wanajeshi sita wa Nigeria wauawa katika shambulizi la kuvizia

    .

    Jeshi la Nigeria linasema wanajeshi sita wameuawa na wanamgambo katikati mwa Jimbo la Niger.

    Wanajumuisha maafisa wakuu wawili na wafanyikazi wengine wanne.

    Uthibitisho huo ulitolewa siku mbili baada ya shambulizi dhidi ya timu ya doria iliyokuwa eneo ambalo majambazi wanaendesha shughuli zao katika eneo la Kati la Nigeria.

    Wanajeshi hao waliripotiwa kupigwa risasi na kufariki katika shambulizi la kuvizia walipokuwa wakiitikia wito baada ya kupigiwa simu ya kuomba msaada Ijumaa usiku.

    Taarifa za ndani zinasema afisa mmoja wao pia alitekwa nyara, lakini jeshi halijathibitisha hilo.

    Katika taarifa yake, msemaji wa jeshi Jenerali Onyema Nwachukwu alisema wanajeshi hao waliwaua washambuliaji kadhaa na kukamata baadhi ya vifaa vyao.

    Haijabainika ni nani aliyetekeleza shambulizi hilo. Nigeria na baadhi ya majirani zake wanaendelea kukabiliana na mashambulizi mabaya ya wanajihadi.

    Pia inakabiliwa na unyanyasaji mkubwa wa majambazi ambao hujihusisha na utekaji nyara ili kupata fidia.

    Shambulizi la hivi punde lilitokea wakati Nigeria ikijiandaa kuandaa mkutano wa kilele wa ngazi ya juu wa Afrika dhidi ya ugaidi mjini Abuja.

    Soma zaidi:

    Mwaka mmoja baada ya kifo cha Abubakar Shekau: Mashambulizi 12 mabaya zaidi ya Boko Haram nchini Nigeria ambayo hayatasahaulika.

  16. Netanyahu aapa kukataa vikwazo vyovyote kwa jeshi la Israel

    Israeli Prime Minister Benjamin Netanyahu. File photo

    Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu ameapa kukataa vikwazo vyovyote kwa jeshi la nchi hiyo, baada ya ripoti kuwa Marekani inapanga kupunguza msaada kwa kitengo kimoja.

    "Nitapambana nayo kwa nguvu zangu zote," waziri mkuu alisema Jumapili.

    Hapo awali, tovuti ya habari ya Axios ilisema Marekani italenga kikosi cha Netzah Yehuda cha Israel kwa madai ya ukiukaji wa haki za binadamu katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu.

    BBC inaelewa kuwa hatua yoyote itafanyika chini ya marufuku ya Marekani ya misaada kwa vitengo vya kigeni vinavyohusishwa na ukiukaji.

    Alipoulizwa wiki iliyopita kuhusu ripoti kwamba msaada wa kijeshi wa Marekani kwa vitengo vya Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) unaweza kupunguzwa kutokana na madai ya ukiukwaji wa haki za binadamu katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu, Waziri wa Mambo ya Nje Antony Blinken alisema: "Nimefanya maamuzi; unaweza kutarajia kushuhidia katika siku zijazo".

    Marekani - mshirika mkuu wa Israel - haijawahi kusimamisha msaada kwa kitengo cha IDF siku za nyuma.

    Jeshi la Israel lilisema Netzah Yehuda ilikuwa inafanya kazi kwa mujibu wa sheria za kimataifa.

    "Kufuatia machapisho kuhusu vikwazo dhidi ya kikosi hicho, IDF haifahamu suala hilo," jeshi limenukuliwa likisema na shirika la habari la Reuters. "IDF inafanya kazi na itaendelea kufanya kazi kuchunguza tukio lolote lisilo la kawaida kwa njia ya vitendo na kwa mujibu wa sheria."

    Waziri wa Ulinzi wa Israel Yoav Gallant aliitaka Marekani kuondoa nia yake ya kuiwekea vikwazo Netzah Yehuda, akisema dunia inaangalia uhusiano kati ya Marekani na Israel kwa karibu zaidi kuliko hapo awali.

    "Jaribio lolote la kukosoa kitengo kizima linasababisha kufuatiliwa kwa karibu vitendo vya IDF," taarifa kutoka kwa Bw Gallant ilisema, na kuongeza "hii sio njia sahihi kwa washirika na marafiki".

    Soma zaidi:

    Shambulizi la Israel Iran: Uharibifu waonekana katika kambi ya anga ya Isfahan

    Isfahan - mji wa kimkakati wa Iran ambapo milipuko ilisikika

    Je,shambulio la Israel dhidi ya Iran linaonyesha nchi hizo hazifahamu uwezo wa kila mmoja kijeshi?

  17. Hujambo na karibu katika matangao yetu ya moja kwa moja ikiwa ni tarehe 22/04/2024