Upinzani waruhusiwa kukagua mitambo ya tume ya uchaguzi Kenya

Bw Odinga amewasili kesi mahakamani kupinga ushindi wa Bw Kenyatta

Chanzo cha picha, Reuters

Maelezo ya picha, Bw Odinga amewasili kesi mahakamani kupinga ushindi wa Bw Kenyatta

Mahakama ya Juu nchini Kenya imeuruhusu muungano wa upinzani nchini humo National Super Alliance (Nasa) kupekua sava zilizotumiwa na tume ya uchaguzi nchini humo wakati wa uchaguzi uliofanyika tarehe 8 Agosti.

Mahakama hiyo imesema muungano huo utaweza kusoma data kwenye sava hizo chini ya uangalizi kuhakikisha usalama wa mitambo ya IEBC hauhujumiwi.

Mgombea wa Nasa Raila Odinga amewasilisha kesi mahakamani kupinga ushindi wa Rais Uhuru Kenyatta wa chama cha Jubilee.

Mawakili wa Bw Odinga wameruhusiwa na mahakama kunakili data kutoka kwenye sava hizo kwa ajili ya kufanya uchunguzi kuhusu uchaguzi huo.

Miongoni mwa mengine, upinzani utapata utambulisho wa sava zilizotumiwa wakati wa uchaguzi, ukuta wa kinga uliotumiwa kulinda sava hizo pamoja na mitambo ya dijitali ya uchaguzi wa Kenya (KIEMS) dhidi ya wadukuzi na mfumo endeshi wa mitambo hiyo pamoja na nywila zilizotumiwa kuingia katika mitambo hiyo.

Kadhalika, wataweza kupata taarifa kuhusu yaliyojiri katika mitambo hiyo ya uchaguzi kuanzia Agosti tano hadi leo.

Aidha, wataruhusiwa kusoma nakala za Fomu 34A na 34B (fomu za matokeo katika vituo vya kupigia kura na ngazi ya maeneo bunge) ambazo zilitumiwa kutangaza matokeo.

Taarifa kuhusu mchakato wa upinzani kupekua sava na mitambo hiyo ya IEBC itawasilishwa kwa mahakama hiyo kesho jioni.

Majaji saba wa mahakama hiyo ya juu wameanza kusikiliza kesi hiyo iliyowasilishwa na Bw Odinga leo.

Kwa mujibu wa matokeo ya IEBC, Rais Kenyatta alipata kura 8,203,290 huku naye Raila Odinga akipata kura 6,762,224.

Samahani, kisakuzi chako hakiwezi kuonesha ramani hii

Tarehe muhimu kesi ya kupinga uchaguzi wa rais

  • Agosti 18: Siku ya mwisho ya kuwasilisha kesi
  • Agosti 20: Siku ya mwisho ya kuwasilisha nyaraka za kesi kwa wanaofaa kujibu kesi
  • Agosti 24: Siku ya mwisho kwa wanaofaa kujibu kesi kuwasilisha majibu
  • Septemba 1: Siku ya mwisho kwa Mahakama ya Juu kutoa uamuzi.

Uamuzi wa Mahakama ya Juu kuhusu kesi hiyo ni wa mwisho. Kwa mujibu wa Katiba ya kenya, iwapo mahakama hiyo itaidhinisha ushindi wa Bw Kenyatta kiongozi huyo ataapishwa kuongoza kwa muhula mwingine tarehe 12 Septemba, siku saba baada ya kutolewa kwa uamuzi.

Iwapo mahakama hiyo itakubali malalamiko ya upinzani na kubatilisha ushindi wa Bw Kenyatta, basi uchaguzi mpya utafanyika katika kipindi cha siku 60 baada ya uamuzi kutolewa, kufikia tarehe 31 Oktoba.

Takwimu kutoka IEBC